March 24, 2012

UTAKWENDA KUJIEREZA MBERE

Ni  kijana  anaedaiwa  kuwa  muhalifu.  hapo  akiwa  katika  bebabeba  ya  tutakwenda


AIBU SANA!!!

Muhindi  kafumaniwa  na  mke  wa  mtu.  ila  swali  linabaki  kwangu  je  mpango  wa  kutembezana  uchi  ndio  maadli  ya  kiafrika.  tena    hii  ni  tabia  ambayo  ni  sawa  na  ngozi  ya  mwili.  wengi  wenu  mnapenda  kuwa  na  kamsemo  ngoja  tumkomeshe  ili  iwe  fundisho  kwa  wengine.  bila  kujua  hata  nyie  mliomfumania mko  katika  kundi  lao  kiujumla  hata  nyie  mnahaibika.  watanzania  kueni  waungwana  na  kufuata  maadili  ya  kiafrika.

March 23, 2012

MOTOR VECO KIGAMBONI

Kivuki  hiki  je  kina  life  jaketi?         swali  kwenu  mamlaka  ya  bandari.  msije  mkatuambia  kuwa  hamkujiandaa,   kiukweli  ni  kwamba    kila  siku  mnasubiri  ajali  zitokee  ndipo  muanze  kukumbuka  kuwa  kuna  usalama  kwanza.

UZALENDO

Mfanyakazi wa kampuni ya Clouds Media, Said Bonge 'Bonge' akirekebisha singe kwenye mnara wa askari katika makutano ya mtaa wa Samora na Azikiwe Dar es Salaam jana. Singe hiyo ilikunjwa wiki iliyopita na mtu anayedaiwa kuwa ni mgonjwa wa akili aliyetaka kuiangusha sanamu hiyo inayolitambulisha jiji la Dar es Salaam.(Na Mpigapicha wetu)

March 22, 2012

Serikali yamjibu Lowassa >

 

YASEMA AJIRA KWA VIJANA SIYO BOMU, WAZIRI KABAKA AMWAGA TAKWIMU, AELEZA MAANA YA AJIRA
Geofrey Nyangoro
SERIKALI imetoa takwimu za ajira kwa vijana nchini  ikiwa ni majibu kwa kauli za mara kwa mara za Waziri Mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa ambaye amekuwa akisema tatizo hilo ni kubwa akililinganisha na bomu linalosubiri kulipuka.
Lowassa amenukuliwa katika matukio manne tofauti kuanzia mwishoni mwa mwaka jana na mwaka huu, akionya tatizo hilo la ajira kwa vijana kwamba linahitaji kupatiwa ufumbuzi wa haraka.

Jana, Waziri wa Kazi na Ajira alisema tatizo hilo haliwezi kufafanishwa na bomu na kusema wanaosambaza uvumi huo hawaitendei haki Serikali, kwani tatizo hilo limepungua kutoka asilimia 12.9 mwaka 2000/1 hadi asilimia 11.7, mwaka 2006.

Katika mkutano wake na waandishi wa habari uliofanyika ofisini kwake Dar es Salaam jana, Kabaka alitoa ufafanuzi wa hali ya ajira nchini na hatua ambazo Serikali inachukua kushughulikia tatizo hilo.
“Hali halisi ya ukuaji wa uchumi nchini ni nzuri lakini, haiwezi kuonekana kama wananchi wake ni maskini na hawana ajira. Hata hivyo, Serikali imekua ikichukua hatua mbalimbali kushughulikia suala hilo ikiwamo la kuhimiza uwekezaji nchini,” alisema Kabaka na kuongeza:

“Kitendo cha wanasiasa kuendelea kusema tatizo la ajira kwa vijana ni bomu linalosubiri kulipuka, siyo kweli na kudai Serikali hayaijafanya kitu wanakuwa hawaitendei haki.”
Alisema utafiti uliofanywa na wizara yake kwa kushirikiana na Taasisi ya Takwimu ya Taifa (NBS), unaonyesha kuwa tatizo hilo limepungua kwa asilimia 1.2.

Mikakati
Waziri Kabaka alisema utafiti uliofanywa na NBS mwaka 2006 ikishirikiana na wizara hiyo unabainisha kuwa nguvu kazi ya Tanzania ni 20.6milioni kati ya watu 37.5 milioni, kwa wakati huo.

Alisema kutokana na utafiti huo, watu 18.3milioni sawa na asilimia 88.3 ya watu hao 20.6milioni walikuwa na ajira huku waliokuwa kwenye ajira ya sekta rasmi wakiwa ni 17milioni sawa na asilimia 92.7.

Kabaka alisema katika utafiti huo, watu 1.3milioni walikuwa kwenye ajira isiyo rasmi huku utafiti ukibaini kuwa kila mwaka watu 800,000 hadi milioni moja wanaingia kwenye soko la ajira.

“Utafiti unaonyesha hali ya ukosefu wa ajira nchini umeshuka kidogo kutoka asilimia 12.9 mwaka 2000/1 na kufikia asilimia 11.7 mwaka 2006, hata hivyo kiwango hicho ni cha juu kwa nchi kama Tanzania ambayo haina huduma za kinga kwa watu wasio na ajira,” alisema Kabaka.

Waziri Kabaka alisema pamoja na kushuka kwa kiwango cha ajira, bado kiwango cha ukosefu wa ajira ni kikubwa huku kikitofatutiana baina ya kundi moja na jingine akisema Tanzania siyo kisiwa hivyo, tatizo linaloikumba dunia la ukosefu wa ajira pia linaikumba nchi hiyo.

Alitaja mikakati ya Serikali kuwa ni pamoja na utekelezaji wa mipango mbalimbali yenye lengo la kukuza ajira ambayo ni pamoja na mpango wa mafunzo yenye kuwezesha vijana kujiajiri, mfuko wa maendeleo ya vijana, mpango wa kukuza ajira kwa vijana na mpango wa uwezeshaji wananchi kiuchumi na kukuza ajira.

Kabaka alitaja mipango mingine kuwa ni ule wa uwekezaji katika elimu na mafunzo, kujengea uwezo mamlaka za Serikali za mitaa (LGAs) na ajira za moja kwa moja zinazotolewa na Serikali kupitia sekta mbalimbali.

“Serikali imetoa ajira kwa walimu 15,000 wa shule za sekondari na msingi na pia kwa kipindi cha miaka mitano 2007 hadi 2011, ajira 414,679 zimepatikana kupitia Kituo cha Uwekezaji (TIC),” alisema Kabaka.

Waziri Kabaka alibainisha mpango kabambe uliowekwa na Serikali katika kukabiliana na tatizo la ajira, ambao alisema hadi kufikia mwaka 2015, itakuwa imepunguza tatizo la ajira kutoka asimilia 11.6 ya mwaka 2006 hadi kufikia asilimia tano.

Alisema katika kutekeleza hilo, Serikali imeanza kuchukua hatua na kwamba imeanda programu ya kwanza itakayolenga kutambua vijana wote wenye taaluma  aina ya ujuzi walionao katika kila wilaya hapa nchini.

“Programu hii ambayo utekelezaji wake unatarajia kuanza mwaka wa fedha wa 2012/13, imejikita katika kuwatambua vijana na shughuli zao ili kuwajengea uwezo katika kukuza tabia ya kijasiriamali, kuwawezesha kupata ujuzi wa kujiajiri na kukuza soko la bidhaa za ndani kwa kuweka mazingira kutumia bidhaa za Tanzania,” alisema Kabaka.

Alisema pia mpango huo umejikita kuwezesha kijana mmojamoja au kikundi kujiajiri, vijana wasomi na wenye ujuzi wanaohitimu katika vyuo vya elimu ya juu kujiajiri na kutengeneza mazingira ya kuajiri wengine na pia kuwezesha sekta binafsi na taasisi za umma kuwekeza katika sekta zenye kipaumbele katika kutoa ajira.

Waziri Kabaka alisema Serikali imejipanga kutekeleza mpango wa kukuza ajira katika maeneo ya mikoa na wilaya ili kuwezesha kupunguza tatizo la ajira na kuwafanya vijana wasikimbilie mijini.

Maana ya ajira
Akinuuku tafsiri inayotumika duniani na kutambuliwa na Shirika la Kazi la Kimataifa (ILO), Waziri Kabaka alisema maana ya ajira ni shughuli yoyote halali anayoifanya mtu mwenye umri wa kufanya kazi kwa kujipatia kipato na kwa kawaida shughuli hiyo ni ya hiari inayotambuliwa kisheria na hufanywa kwa saa 40 hadi 45 kwa wiki.

Alisema ukosefu wa ajira ni hali ambayo hutokea wakati watu walioko kwenye umri wa kufanya kazi na ambao wangependa kufanya kazi wanatafuta bila ya kuipata.

“Tafisiri hii ya kimataifa haiwajumuishi wale wasiotafuta kazi, wasiopenda kufanya kazi hata kama hawana kazi,” alisema Kabaka na kuongeza:
“Lakini tafisiri inayotumika zaidi Tanzania inatambua wote wasio na kazi na ambao wako tayari kufanya kazi  bila kujali wanatafuta kazi au la na inawahusisha hata  wasio na uhakika wa kufanya kazi hata ya siku moja.”
Alitaja aina tatu za ajira ambazo ni kazi ya staha, kazi chini ya kiwango na ajira maskini.

Alisema ajira za staha ni zile ambazo zina tija kiusalama, heshima haki za wafanyakazi na kipato cha kutosha, wakati ya ile ya chini ya kiwango ni ile ambayo haitoshelezi kutumia uwezo, muda na taaluma yote ambayo ambayo mhusika anayo. Ajira maskini ni ile ambayo kipato kinachopatikana ni cha chini ya kiwango kisichomwezesha mtu kuishi.

Akirejea utafiti wa ILO wa mwaka 2010/11, Waziri Kabaka alisema ripoti hiyo inaonyesha hali ya umaskini na ukosefu wa ajira duniani ni kubwa. Watu 205 milioni dunia kote mwaka 2010 hawakuwa na ajira.
Alisema idadi hiyo ilikuwa sawa na ongezeko la nguvu kazi isiyo na ajira duniani ya watu 27.7 milioni kulinganisha na ile ya mwaka 2007.

Alisema sababu za ongezeko la ukosefu wa ajira kwa mujibu wa ripoti hiyo, ni kutokana na utandawazi, maendeleo ya mawasiliano, mabadiliko ya teknolojia ambayo hayahitaji nguvu kazi nyingi katika utendaji kazi na kudidimia kwa nguvu za kiuchumi hasa katika nchi zinazoendelea.

Lowassa na ajira
Novemba 15, mwaka jana akiwa katika harambee ya ujenzi wa Kanisa Katoliki la Mtakatifu Joseph Makasa, Parokia ya Nyakato, Mwanza, Lowassa alionya kuhusu tatizo hilo na kulitaka lisaidie kujenga vyuo vya ufundi.

Alitoa takwimu akisema utafiti wa mwaka 2006, ambao hata hivyo, hakusema ulifanywa na taasisi gani, ulionyesha tatizo hilo kwa sasa limekuwa na kufikia asilimia 15 huku likigusa zaidi vijana wenye umri wa miaka kati ya 15 hadi 24 ambao ndiyo nguvukazi ya taifa... “Ninapozungumza hili siyo nia yangu kumlenga mtu. Mimi ni Yohana Mbatizaji, hii ni sauti inayolia nyikani.”

Novemba 29, mwaka huo wa jana akiwa harambee ya ujenzi wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri (KKT), Usharika wa Amani Sabasaba, Singida, Lowassa alirudia tena suala hilo la tatizo ajira.

Mapema mwaka jana, Lowassa pia alifanya mkutano na waandishi wa habari Mjini Arusha na kuzungumzia tatizo hilo la ajira ambalo alilifananisha na bomu.

Jumatatu iliyopita, Lowassa alirejea kauli hiyo alipokuwa katika sherehe za uzinduzi wa Jimbo jipya la Kanisa Katoliki Ifakara akisema: “Nawaomba maaskofu katika miradi yenu mlipe kipaumbele suala la tatizo la ajira kwa vijana.... hili kama tulivyosema ni bomu linalosubiri kulipuka...

March 21, 2012

Shirika la Umeme Tanzanian lapata mkopo kuzuia kukatika kwa umeme:











Benki tatu zimekubali kutoa mkopo wa shilingi bilioni 408 (Dola za Marekani 256) kwa Shirika la Umeme Tanzania kwaajili ya mpango wa dharula wa kuzuia kukatika kwa umeme, gazeti la Daily News la Tanzania liliripoti Jumatatu (tarehe 19 Machi).Fedha hizo zitasaidia kununua mafuta mazito kwaajili ya mitambo inayotumia mafuta mazito hayo, alisema William Mhando, mkurugenzi mkuu wa Shirika la Uzalishaji na Ugavi wa Umeme Tanzania (TANESCO). "Tunatarajia kupata fedha hizo wili lijalo."
Kampuni inafanya kazi katika "changamoto ya muda" kukarabati miundombinu ya umeme nchi nzima, Mhando alisema, aliongeza kwamba uzalishaji umeshuka hadi megawati 718 kutoka megawati 1200. Alisema shirika la umeme halifanyi mgao wa umeme na tatizo lolote linatokana na mfumo mbaya wa miundombinu. "Hakukuwa na uwekezaji madhubuti katika eneo hili kwa muda mrefu," alisema.
City Bank Tanzania, National Microfinance Bank na National Bank of Commerce zinatoa mkopo kwaajili ya mradi huo.

Mwakyembe: Sijafa, nitabaki hai

Naibu Waziri wa Ujenzi, Dk. Harrison Mwakyembe, akiingia kwenye ofisi za wizara hiyo tayari kuanza kazi jana na baadaye kuzungumza na waandishi wa habari. Dk. Mwakyembe, alirejea nchini Ijumaa iliyopita

















Naibu Waziri wa Ujenzi, Dk. Harrison Mwakyembe, amesema waliokuwa wanataka kuandika kichwa cha habari kuwa amekufa sasa wajue yuko hai, na ametaka mjadala kuhusu kuugua kwake ufungwe kwa sababu umekuwa unaiumiza na kuiathiri sana familia yake.
Alisema hayo jana alipozungumza na waandishi wa katika makao makuu ya Wizara ya Ujenzi, jijini Dar es Salaam, muda mfupi baada ya kuripoti ofisini kwake kuendelea na kazi baada ya afya yake kuimarika kutokana na kuumwa kwa miezi kadhaa.
Dk. Mwakyembe ambaye ni Mbunge wa Kyela (CCM), aliingia ofisini kwake jana saa 3.57 asubuhi na baadaye kuzungumza na waandishi kwa dakika zisizopungua 10, kuanzia saa 4.20 asubuhi.
Alisema mjadala kuhusu kuugua kwake, umekuwa ukishupaliwa na baadhi ya magazeti kwa kuupamba kwa vichwa vizuri vya habari ili kufanya biashara.
“Lingine tu ambalo pengine waandishi wa habari niwaeleze, lakini niwaombe vilevile, jamani sasa suala la Mwakyembe kuumwa basi lifike basi mwisho,” alisema Dk. Mwakyembe, ambaye alirejea nchini Ijumaa iliyopita kutoka kwenye matibabu nchini India.
Aliongeza: “Unajua kwenye Journalism (uandishi wa habari) lazima mtu pia ujali hali inayowahusu watu wengine. Nina watoto. Sasa kila siku huyu baba ambaye anategemewa kufa kesho asubuhi hata kama inaleta headline (kichwa cha habari) kizuri kwenu na kuuza gazeti inaumiza.”
“Mliopenda kupata headline (kichwa cha habari) kwamba nimekufa, basi niko hai na nitaendelea kuwa hai. Kwa hiyo nawaombeni jamani yaishe tafadhali, nawaombeni sana,” alisema.
Alisema alikuwa anaumwa, lakini sasa amerudi kutoka nchini humo alikokuwa amekwenda kupata matibabu akiwa mzima na anaendelea na kazi.
“Nilikuwa naumwa, kwa kweli nimerudi sasa mimi ni mzima kabisa, naendelea na kazi, mmenikuta ofisini kwangu. Na sasa hivi ningependa nifanye kikao kiwe kifupi zaidi maana nina mafaili lundo yananisubiri kuweza kuyapitia,” alisema Dk. Mwakyembe.

AWASHUKURU JK, MAGUFULI, WATANZANIA
Aliishukuru serikali, hasa Rais Jakaya Kikwete, kwa kubeba jukumu hilo hadi kwenda kumuona nyumbani kwake na kushinikiza apata matibabu haraka iwezekanavyo.
Pia aliishukuru serikali kwa kuhakikisha amepata usafiri uliomuwezesha kwenda hospitali nchini India.
Vilevile, alimshukuru Waziri wa Ujenzi, Dk. John Magufuli, Katibu Mkuu, Balozi Herbert Mrango na Naibu Katibu Mkuu Wizara hiyo, Dk. John Ndunguru, kwa kuendesha wizara peke yao bila msaada wake.
Kadhalika, aliwashukuru wananchi wote nchini, wakiwamo Wakristo na Waislamu, waliojitolea kumuombea apate afya njema.
“Maombi yao hayakuwa ya bure, yamezaa matunda, mimi sasa hivi ni mzima na naendelea na kazi,” alisema Dk. Mwakyembe.


Akijibu swali kwamba uchunguzi wa madaktari umeonyesha alikuwa akisumbuliwa na tatizo gani, alisema anaiachia serikali kupitia tume iliyoiunda kueleza suala hilo.  



“Kwa sababu nilipokuwa India nikaambiwa kuwa Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ameunda tume inachunguza. Tuiache serikali. Kwa hiyo, kama kuna lolote ninalo nitaieleza serikali, na kama kuna taarifa yoyote nitaipa hii tume ambayo Waziri wa Mambo ya Ndani amesema,” alisema Dk. Mwakyembe.

AWATAKA WAPIGAKURA KYELA
KUSITISHA MAANDAMANO

Aliwashukuru wapigakura wa Jimbo la Kyela mkoani Mbeya, ambao walipanga kuandamana kwenda jijini Dar es Salaam kumuona Rais Kikwete ili waelezwe maradhi yaliyokuwa yanamsumbua Dk. Mwakyembe.
“Kwanza nitangulie kwa kuwashukuru sana. Kwanza kwa maombi yao na vilevile subira kubwa waliyokuwa nayo katika kipindi chote ambacho mbunge wao nimekuwa sipo,” alisema Dk. Mwakyembe.
Aliongeza: “Naomba niwahakikishie tu wana Kyela hawana haja ya kuandamana tena, nimekuja. Napanga kwenda Kyela mimi mwenyewe katika wiki moja mbili zijazo kufuatana na lundo la kazi litakalopungua hapa wizarani.”
Kuhusu kupishana kauli kati yake na Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI), Kamishna Robert Manumba, Dk. Mwakyembe alisisitiza kuwa hawezi kurejea tena suala hilo kwa vile linashughulikiwa na serikali.
“Serikali imeamua kulichunguza hili suala. Sasa hatuwezi kuendesha parallel systems (mifumo sambamba). Serikali inachunguza halafu sisi huku kama waandishi wa habari tunaongea haya, haitokuwa sahihi,” alisema Dk. Mwakyembe.
Aliongeza: “Tuiache serikali iangalie hili suala, maana nikisema serikali ni pamoja na hata yeye DCI Manumba, polisi wote wanahusika. Kwa hiyo, hebu tuipe nafasi serikali ije na taarifa ambayo pengine itaturidhisha wote.”
“Lakini kwa upande wangu mimi kama Mwakyembe, mimi kama nilivyosema siku nyingi namuachia Mungu. Na tuiachie serikali.”

‘UGONJWA WAKE NI WA KITAALAMU’
Alisema hawezi kuwaeleza Watanzania ugonjwa unaomsumbua hawataelewa kwa sababu ni mambo ya kitaalamu.
“Hata kama watu watakimbilia kuuangalia (ugonjwa huo) kwenye kamusi hawawezi kufanikiwa kupata chochote,” alisema Dk. Mwakyembe.
Dk. Mwakyembe amekuwa akisumbuliwa na maradhi ya ngozi ambayo Oktoba 9, mwaka jana, yalimlazimu kupelekwa katika Hospitali ya Appolo, India kwa matibabu zaidi.
Maradhi hayo yalizua utata mkubwa baada ya kudaiwa kuwa yametokana na kuwekewa sumu, huku kukiwa na kauli mbalimbali zinazotofautiana kutoka kwake na baadhi ya watendaji wengine wa serikali.
Kauli tata zaidi ziliibuka baada baadhi ya viongozi, akiwamo Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samwel Sitta, kudai kuwa maradhi yanayomsumbua Dk. Mwakyembe yametokana na kulishwa sumu.
Hata hivyo, Kamishna Manumba alijibu madai hayo aliposema kuwa uchunguzi wa polisi umebaini kuwa Dk. Mwakyembe hajaugua kwa sababu ya kulishwa sumu na kutishia kuwachukulia hatua waliotoa kauli hizo.
Ripoti ya uchunguzi aliyoisoma Manumba katika mkutano wake na waandishi wa habari Februari 16, mwaka huu, jijini Dar es Salaam, inaonyesha kuwa Dk. Mwakyembe hakulishwa sumu huku akisema kwamba pia ilijumuisha taarifa kutoka hospitalini India ambako alikuwa anatibiwa.
Alisema uchunguzi huo unalipa Jeshi la Polisi picha kuwa waliotoa taarifa hizo hadharani wanapaswa kuchukuliwa hatua za kisheria.
Baada ya kauli hiyo, Dk. Mwakyembe aliibuka na kutoa kauli nzito iliyoonekana kumjibu Kamishna Manumba akielezea kushangazwa kwake na majibu hayo, huku akisisitiza kuwa madaktari waliokuwa wakimtibu walikuwa wakitafiti chanzo cha  ugonjwa wake na walikuwa hawajafikia hitimisho, hivyo si sahihi kwa Manumba kusema kuwa hautokani na kulishwa sumu, kwani sumu si lazima ikudhuru kwa kulishwa tu.
Mbali ya Dk. Mwakyembe, Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Haji Mponda, na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Shamsi Vuai Nahodha, kwa nyakati tofauti walikana kuijua ripoti hiyo ya Kamishna Manumba.
Hata hivyo, katika kile kilichoonekana kudhamiria kuchukua hatua, Kamishna Manumba aliwasilisha jalada la mashtaka kwa watu hao kwa Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), Eliezer Feleshi, ambaye alithibitisha kupokea jalada hilo, lakini alisema ni vigumu kufahamu ni lini atakapopeleka mahakamani jalada la kesi dhidi ya watu hao.